Ads

ACT Wazalendo Waeleza Ukuaji wake Kuelekea Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024

Na Francisco Peter

Chama Cha ACT Wazalendo kupitia Kamati Kuu yake kimeielekeza Sekretarieti kuandaa midahalo ya wazi ya wagombea wa Chama na Ngome za Wanawake na Vijana ili kuwatambulisha kwa wanachama na umma kupitia sera zao.
Akizungumza na waandishi wahabari Jijini Dar es Salaam Naibu Katibu wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma wa Chama hicho Janeth Rithe amesema maazimio hayo ni matokeo ya Kikao Cha Kamati Kuu kilichokaa Jijini Dar es Salaam Januari 27 mwaka huu.

Aidha ameainisha maazimio ya kamati Kuu kuwa ni pamoja na, chaguzi za mikoa na majimbo, maboresho ya Kalenda ya Mkutano Mkuu Taifa, maboresho ya Katiba ya Chama na Sera ya Usawa wa Kijinsia na Uteuzi wa Makatibu wa Mikoa na Majimbo.

Kuhusu chaguzi za Mikoa na Majimbo, Rithe ameeleza kuwa Kamati Kuu ilipokea Taarifa ya Uchaguzi wa Chama katika ngazi ya Mikoa na Majimbo. 

Kwa upande wa Bara, Majimbo yote 214 yamefanya uchaguzi sawa na asilimia 100 na Mikoa yote ya Kichama 28 imefanya uchaguzi sawa na asilimia 100.

“Vilevile, kwa upande wa Zanzibar, Majimbo yote 50 yamefanya uchaguzi sawa na asilimia 100 na Mikoa yote ya Kichama 11 imefanya uchaguzi sawa na asilimia 100. Kamati Kuu imeipongeza Sekretarieti ya Chama kwa kukamilisha chaguzi za Majimbo na Mikoa kwa asilimia 100,”. 

Rithe ameeleza kwamba hatua hii ni kiashiria cha wazi cha ukuaji wa kasi wa Chama cha ACT Wazalendo katika kipindi hiki muhimu kuelekea Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024 na Uchaguzi Mkuu 2025.

Kwa upande wa maboresho ya Kalenda ya Mkutano Mkuu Taifa, amesema Kamati Kuu ya Chama Taifa, baada ya kupokea na kujadili Taarifa ya Maandalizi ya Mkutano Mkuu Taifa, iliidhinisha kuwa Mikutano Mikuu ya Chama ifanyike kama ifuatavyo, Mkutano Mkuu wa Ngome ya Vijana Februari 29, 2024, Mkutano Mkuu wa Ngome ya Wazee Machi1, 2024.

Mikutano mingine ni Mkutano Mkuu wa Ngome ya Wanawake Machi 2, 2024, Mkutano Mkuu Taifa Machi 5-6, 2024 huku Mkutano wa hadhara wa Kutangaza viongozi wa Chama waliochaguliwa ukipangwa kufanyika Machi 6 mwaka huu.

Kuhusu, maboresho ya Katiba ya Chama na Sera ya Usawa wa Kijinsia amebainisha kwamba Kamati Kuu imepokea Rasimu ya kwanza ya maboresho ya Katiba ya ACT Wazalendo iliyowasilishwa na Mwanasheria Mkuu wa Chama baada ya kukusanya na kuchambua maoni ya wanachama. 

Kwamba Kamati Kuu, baada ya majadiliano ya kina imeelekeza Rasimu hiyo, baada ya maboresho kwa kuzingatia maoni ya Kamati Kuu, ipelekwe Halmashauri Kuu kwa ajili ya kupokea maoni zaidi kabla haijawasilishwa Mkutano Mkuu Taifa kwa ajili ya kuidhinishwa.

Vilevile, ameeleza kuwa Kamati Kuu imepokea Rasimu ya Sera ya Jinsia inayolenga kuhakikisha uwakilishi mpana zaidi wa wanawake kwenye vyombo vya maamuzi ndani ya Chama na katika chaguzi za kiserikali unazingatiwa. Kamati Kuu imeelekeza kuwa Rasimu hiyo, baada ya maboresho kwa kuzingatia maoni ya Kamati Kuu, ipelekwe Halmashauri Kuu ya Chama Taifa kwa ajili ya kuidhinishwa.

Katika hatua nyingine, Kamati Kuu ilipokea Rasimu ya Sera ya Kuwaenzi Viongozi Wastaafu waliokitumikia Chama kwa heshima, bidii na utii. Baada ya majadiliano ya kina, Kamati Kuu iliridhia Sera hiyo iwasilishwe Halmashauri Kuu kwa ajili ya kuidhinishwa.

Kwenye uteuzi wa Makatibu wa Mikoa na Majimbo, Rithe amesema, Kamati Kuu Taifa kwa kuzingatia madaraka yake chini ya Ibara ya 79 (vii) ya Katiba ya ACT Wazalendo imefanya uteuzi wa Makatibu wa Mikoa yote ya Tanzania Bara isipokuwa Pwani ambapo uteuzi huo utafanyika wakati mwingine na Zanzibar imefanyika kwa mikoa yote.

No comments