Ads

BoT YAWAJENGEA UWEZO VIONGOZI WA DINI KUTAMBUA FEDHA HALALI

NA NOEL RUKANUGA, DAR ES SALAAM

Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imewataka viongozi wa dini wakiwemo maskofu, mashehe, mapadre pamoja na wachungaji kutoa elimu kwa waumini kutoka dini mbalimbali kuhusu matumizi sahihi ya noti na sarafu, kutambua fedha bandia jambo ambalo litasaidia kupunguza gharama za kutengeneza fedha ambazo zinaharibika kutokana na matumizi mabaya.

Akizungumza leo Disemba 11, 2023 jijini Dar es Salaam wakati wakitoa mafunzo ya utunzaji wa Noti na Sarafu kwa Kamati ya Amani Mkoa wa Dar es Salaam, Meneja Msaidizi Shughuli za Uendeshaji wa Noti na Sarufu, Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Bw. Salala Nchunga, amesema kuwa lengo la kutoa elimu kwa viongozi wa dini ili kufikia ujumbe kwa watanzania kuhusu umuhimu wa kutunza fedha.

Bw. Nchunga amesema kuwa fedha zinapita katika mikono mingi ikiwemo katika nyumba za ibada kupitia kwa waumini kutoka dini mbalimbali wakati wa kutoa sadaka.


“Tumewafundisha namna ya kutambua alama za fedha halali za kitanzania, utunzaji, matumizi sahihi ya fedha, kwani safaru na noti ikikaa muda mrefu bila kuharibika tunaokoa fedha nyengi” amesema Bw. Nchunga.

Bw. Nchunga amesema kuwa matumizi ambayo sio sahihi ya fedha inasababisha serikali kupata hasara ya kutengeneza fedha mpya.

Amesema kuwa elimu ambayo wametoa kwa viongozi wa dini ya jinsi ya kutunza fedha kwa usahihi, kutambua fedha bandia wanatarajia kuleta tija katika kuhakikisha zinakuwa katika mazingira rafiki.

“Fedha bandia zinavyoongezeka katika mzunguko inapelekea nchi kuanza kufikilia tengeneza fedha ya aina nyengine katika mzunguko” amesema Bw. Nchunga.

Bw. Nchunga ameeleza kuwa BoT ina matawi mengi, hivyo wameanza kutoa elimu katika Mkoa wa Dar es Salaam kutokana kuna mzunguko mkubwa wa kiuchumi, hivyo wanatarajia kuendelea katika Mikoa mengine ili kuhakikisha elimu inafika kwa viongozi wa dini nchi zima.

Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Amani Mkoa wa Dar es Salaam Sheikh Abdallah Iddi, mafunzo waliopata wanakwenda kuleta tija katika utekelezaji wa majukumu hasa kutoa elimu kwa waumini.

Amesema kuwa noti na sarafu ni mali ya nchi kila mmoja ana wajibu wa kuitunza kwa muda mrefu ili mzunguko wa fedha uwe mzuri pamoja na uchumi wa nchini.

“Ni makosa kutumia pesa katika mazingira ambayo sio rafiki ikiwemo kuikanyaga kwa kusababisha kuharibika haraka na kuleta hasara kwa serikali” amesema. 

Hata hivyo ametoa wito kwa BoT kuendelea kutoa elimu kwa umma ili kutambua umuhimu wa kutunza fedha za Tanzania.







No comments