TALGWU, PSI WATOA VITENDEA KAZI KWA WAFANYAKAZI WA KUHIFADHI TAKA NGUMU
NA NOEL RUKANUGA, DAR ES SALAAM.
Chama cha Wafanyakazi wa Serikali
za Mtaa Tanzania (TALGWU) kwa kushirikiana na Taasisi ya Public Service
International (PSI) imewataka wadau mbalimbali kutoa ushirikiano katika
kuhakikisha wafanyakazi wa kuhifadhi taka ngumu wanakuwa katika mazingira
rafiki wakati wakitekeleza majukumu yao.
Kwa kutambua umuhimu wa
wafanyakazi wa kuhifadhi taka ngumu Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mtaa
Tanzania (TALGWU) na Taasisi ya Public Service International (PSI) wametoa
msaada wa vitendea kazi kwa wafanyakazi wa Dampo la Pugu Kinyamwezi na
wakusanya taka ngumu katika soko la buguruni jijini Dar es Salaam.
Akizungumza leo tarehe
5.8.2022 jijini Dar es Salaam na wafanyakazi wa kuhifadhi taka ngumu katika Dampo
la Pugu Kinyamwezi na Buruguni Sokoni, Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa
Serikali za Mtaa Tanzania (TALGWU) Rashid M. Mtima, amesema kuwa wakati umefika
kwa taasisi na wadau mbalimbali kutoa msaada wa vifaa na vitendea kazi kwa wahifadhi
wa taka ngumu kutokana wanafanya kazi katika mazingira magumu.
“Wanapaswa kupewa ushirikiano
kwa kuwapatia vifaa ikiwemo glovu, vazi la kazi, viatu vya kazi waweze kufanya
kazi zao katika mazingira rafiki na kuepukana na mlipuko wa magonjwa” amesema
Bw. Mtima.
Bw. Mtima amesema kuwa TALGWU
inatambua umuhimu wanaofanya kazi ya kukusanya na kuhifadhi taka ngumu, kwani
wengine ni wanachama wao kupitia makampuni zinazosimamia kazi ya kusafisha
mazingira katika maeneo mbalimbali nchini.
Ameeleza kuwa wafanyakzazi
wa serikali za mitaa inajumilisha halmashauri zote nchini, huku taka ngumu zote
za jiji la Dar es Salssm zikipelekwa kuhifadhiwa katika Dampo la Pugu
Kinyamwezi.
Amefafanua kuwa TALGWU
kupitia PSI wana malengo ya kuona kwa namna gani wanaboresha mazingira ya kazi katika
shughuli za kusimamia taka ngumu kuanzia majumbani mpaka eneo la kuhifadhia.
‘Suala la kusimamia taka
ngumu liwe kwa kila mtu hapa nchini na kuona kwa namna gani tunaweza kusaidia
katika kuhifadhi, taka sio jambo la kubeza, hivyo kila mmoja tuna kila sababu
ya kulisimamia” amesema Bw. Mtima.
Hata hivyo wahifadhi taka
ngumu katika Dampo la Pugu Kinyamwezi wameiomba serikali kuweka huduma ya afya
katika eneo hilo jambo ambalo litawasaidia pale watakapo pata changamoto.
Wamesema ni vizuri wadau
mbalimbali wakajitokeza kwa ajili ya kuwapatia vifaa vya kufanyia kazi kutokana
asilimia kubwa wanafanya kazi hiyo bila vitendea kazi na kuhatarisha afya zao.
Wameishukuru Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mtaa Tanzania (TALGWU) na Taasisi ya Public Service International (PSI) kwa kuwapatia vifaa mbalimbali kwa ajili ya kuwasaidia katika kutekeleza majukumu yao.
Post a Comment