Ads

WAZIRI NDALICHAKO ATAKA ORODHA YA MASHIRIKA,TAASISI YASIYOWASILISHA MICHANGO, ATOA MAELEKEZO CHANGAMOTO ZINAZOHUSU WASTAAFU

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri MKuu Kazi,Vijana,Ajira na Watu wenye Ulemavu Profesa Joyce Ndalichako akizungumza mbele ya Wazee wastaafu wa Mkoa wa Dar es Salaam walioko katika mfuko wa NSSF na PSSSF kwa lengo la kusikiliza changamoto zao na kupata ufumbuzi wake,leo Julai 22,2022 katika Ofisi za NSSF Mafao House Ilala jijini DSM

Na Mwandishi Wetu.

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri MKuu Kazi,Vijana,Ajira na Watu wenye Ulemavu Profesa Joyce Ndalichako ametoa maelekezo ya kupata orodha ya mashirika,Taasisi, Halmashauri na majiji ambayo hayawasilishi michongo ya wanachama wa mifuko mbalimbali ya jamii.

Aidha ametumia nafasi hiyo kutoa maelekezo kwa mifuko ya pensheni kutatua changamoto ambazo zinasababisha wastaafu kuchelewa kupata pensheni zao au kupunjwa fedha zao hali inayosababisha kuendelea kwa malalamiko ambayo yangeweza kupata ufumbuzi wa haraka.

Profesa Ndalichako amesema hayo leo Julai 22,2022 alipokutana na wastaafu wa Mkoa wa Dar es Salaam walioko katika Mfuko wa NSSF na PSSSF kwa lengo la kusikiliza changamoto za wastaafu hao na kupata ufumbuzi wake."Leo nimetoa fursa ya kukutana ili kama kuna mtu anachangamoto inayohusiana na mafao ambayo yanalipwa kupitia mfuko wa NSSF na pia NSSF apate fursa ya kuelezea changamoto zake.

"Na lengo la kufanya hivyo ni kutokana na uzoefu niliouna ndani ya miezi sita tangu nimeanza kuwa katika Ofis ya Waziri MKuu , Kazi,Vijana,Ajira na Watu wenye Ulemavu kwani nimekuwa nikipata changamoto mbalimbali za wastaafu ambazo ziko katika makundi tofauti ,zipo changamoto ambazo zinatokana na mapunjo kwa maana ya kwamba mafao ya mtu yamekokotolewa kwa kutumia mshahara ambao ni mdogo kuliko mshahara halisi wa mfanyakazi alipomaliza

"Kwa hiyo inasababisha kwanza mafao ya mkupuo anayopewa yanakuwa kidogo kuliko ilivyotakiwa lakini na pensheni yake ya mwezi inakuwa ni ndogo kuliko inavyotakiwa.Na kwa muda ambao nimeangalia Dodoma na hata hapa leo nimeshawapata watu ambao unaona kabisa kesi yake iko wazi anachotakiwa ni kwenda kurekebishiwa alipwe pensheni kwa kuzingatia mshahara wake wa mwisho na alipwe stahiki zote ambazo alikuwa anapunjwa,"amesema Profesa Ndalichako.

Akifafanua zaidi amesema kwa hiyo hilo ni kundi la kwanza lakini haya mafao yako kwa mujibu wa taratibu mtu anapokuja hapa inatakiwa awe na vielelezo kuonesha ile salari slip yake na pia kuna utaratibu wanaangalia michango iliyokuwa inawasilishwa na waajiri.

"Kwa hiyo unakuta haya ni makosa labda niseme ya kiutendaji watu kutokuwa makini katika kazi kwasababu wako ambao wanachangamoto kama hii na amezunguka na taasisi hiz I nimeshongea na wakurugenzi itabidi waimarishe vile vitengo vyao vya kuwapokea watu.

"Wanaweka ukuta mgumu sana wa wateja kuweza kuwaona wakuu kwa hiyo unakuta vitu ambavyo kama wale watendaji wangekuwa wanaacha wateja wakaone watu ambao Wana maamuzi jambo lingekuwa limekwisha muda mrefu.Lakini unakuta anawazungusha hayupo,amesafiri ,yupo kwenye kikao hata kama yupo wanazuia wasimuone Mtendaji mkuu

"Watendaji wakuu ni watumishi wa umma kama ambavyo mimi Waziri ni mtumishi wa umma, nimeshuka kuja kuwaona wastaafu kwanini na wao wasifanye hivyo ,kwa hiyo nimeelekeza kuta zote za Ofisi wazivunje na milango iwe wazi kusikiliza na kutatua kero za wateja wao.

"Kwahiyo hiyo ni changamoto tutaendelea kuifanyia kazi na naona wengi ambao wanakuja ni suala la mapunjo lakini kuna suala la lingine la mifuko tulipobadilisha sheria ya 2018 kwa hiyo utakuta mtu alihama labda kutoka mfuko wa NSSF akaenda PSSFf au vinginevyo alikuwa PSSF akaenda NSSF,"amesema Profesa Ndalichako.

Amesema sasa hiyo kiutaratibu kama mstaafu alichangia kwenye mfuko uliohamia chini ya miezi 12 atabaki kwenye mfuko wa zamani kama alichangia zaidi ya miezi 12 atahamia kwenye mfuko mpya baada ya marekebisho ya sheria ya mwaka 2018.

"Lakini sasa utakuta kunakuwa na mawasiliano hafifu kati ya mifuko hiyo kwa hiyo unakuta labda michango ya mfuko mmoja kwenda kwenye mifuko mingine inasababisha mstaafu asipate mafao yao.Kwa kuwa tuko wote kwa pamoja hilo tunaliona na tutaendelea kuifanyia kazi na nimeshaawambia watendaji wakuu wasisubiri mpaka mimi niende.

"Baada ya Dar es Salaam kituo kitakachofuata ni Mwanza hivyo waanze kuangalia kwenye mafaili yao maana kuna wengine wameshaandika barua zaidi hata mara sita wamekuja hapa na vielelezo vyao nimeviona a nimeziomba kwa hiyo tufanyie kazi kero ambazo tayari zipo ofisini.

"Nikienda Mwanza nikutane na kero ambazo ni mpya na waache wastaafu kama wanataka kwenda kuwaona viongozi waweze kuwaona ,kwa hiyo nimeona nikutane na wastaafu wangu kwasababu ni maelekezo ya Rais ,sisi wasaidizi wake ni lazima tuhakikishe tunatatua kero ambazo ziko katika maeneo yetu na mimi mheshimiwa Rais amenipatia dhamana ya kuongoza kundi ambalo analiheshimu sana.

"Rais wetu anajali na kuheshimu wazee na hataki kusikia wakihangaika ,Rais hataki kusikia wazee ambao wamelitumikia Taifa kwa weledi,wametufikisha hapa tulikofika halafu leo hii wanasumbuliwa kwa vitu ambavyo ni stahiki yao,najua zipo na changamoto kwenye mashirika kutowasilisha michango kwa wakati na baadhi ya watu ambao hawawasilishi michango ni watu wa Serikali, wakurugenzi wa Halmashauri, Masharika ya umma,"amesema.

Amefafanua kwa hiyo changamoto wameiona na anategemea wiki ijayo kupata orodha yote ya taasisi,halmashauri ,majiji na mashirika ambayo hayawasilishi michango na kwasababu kazi hiyo Rais amemtuma yeye niondoe hiyo kero na ili mtu alipwe mafao yake ni lazima taasisi au kama ni Serikali au kama ni Wizara au nishirika la umma awasilishe michango.

"Wale wote ambao ni taasisi za umma niwasihi walipe michango kwa ajili ya watumishi wao ili mifuko iweze kuwalipa mafao yao mara moja.
Walipe michango ya watumishi ili mifuko iweze kuwalipa mafao na kuanza kuwalipa pensheni zao mara moja na wale ambao hawatalipa nitamkabidhi orodha Mama(Rais) mwenyewe.

"Lakini zipo taasisi binafsi na mashirika ambayo watu wanashindwa kupata mafao yao kwasababu muajiri hajawasilisha michango.Kuna uzembe unaofanyika na kuna ushahidi utaratibu uliokuwa unatumika kama taasisi au Shirika halijawasilisha mafao tulikuwa tunawapeleka mahakamani wanafunguliwa kesi za madai

"naonekana kesi za madai ni nyepesi sana kwa hiyo mtu akishapelekwa mahakamani anasema nitalipa kwa hiyo kunakuwa hakuna kesi ambayo unasema utamfunga,hivyo tuko katika mapendekezo ya kubadilisha sheria na taratibu zetu ili hawa ambao wamekata fedha wanashindwa kuzileta ni jinai kwasababu ule ni wizi.

"Kuna ushahidi amekata fedha lakini hajaleta mchango ,kwa hiyo kunamchakato ambao tunakusudia kuupeleka ndani ya Serikali,tutashirikiana na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ili kuhakikisha tunakuwa na kibano kikali zaidi cha kuhakikisha yale mashirika na sekta binafsi ambao hawawasilishi michango wanabanwa na sheria iliyokali zaidi.

"Kwasababu Sheria ya sasa inawapa nafasi ya kupumua na ndio maana wanazunguka tu kwenye kiti, wanaotembelea magari yenye viyoyozi wakati wastaafu wanateseka hilo jambo tunalifanyia.Kwa hiyo vikao hivi vitakuwa ni endelevu kwasababu kama Dar es Salaam kweli mmeitikia na nimi niwaambie sitoki hapa nitakaa hapa hata kama ni saa sita za usiku niwasikilize wote moja baada ya mwingine,"amesema .

Amesisitiza fomu zote ambazo zimewasilishwa na wastaafu hao ili kutatuliwa changamoto zao zitafanyiwa kazi huku akitoa angalizo wale ambo wanaomba pensheni ziongezwe hilo liko nje ya uwezo wake lakini ameahidi kulifikisha kwenye Mamlaka za juu ili kuona itavyokavyoamriwa."Kuna wengine wanalipwa na mfuko wa Hazina ambao wanaomba kuongezwa kipato chao, hilo liko nje ya uwezo wangu lakini nitafikisha ombi hilo kwa Mamlaka husika.




No comments