Ads

TUME YA MADINI YAKABIDHIWA MAGARI KUBORESHA UTENDAJI KAZI.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendelea kununua vitendea kazi ikiwemo mashine za kupima madini pamoja na kusimamia kwa ukaribu shughuli za madini ili kuhakikisha inapata mapato yake stahiki.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati akikabidhi magari saba kati ya magari 40 kwa Tume ya Madini Waziri wa Madini, Dkt. Doto Biteko amesema kuwa magari hayo ni moja ya mikakati ya kuboresha mazingira ya ukusanyaji wa maduhuli kwenye shughuli za uchimbaji na biashara ya madini nchini.

Dkt. Biteko amesema kuwa magari hayo yatatumika kama kichocheo cha ukusanyaji wa maduhuli kwenye shughuli za uchimbaji na biashara ya madini.

Amewataka watendaji wa Tume ya Madini kuhakikisha magari yanatunzwa na kuendelea kuchapa kazi kwa ubunifu mkubwa ili kuhakikisha lengo la kukusanya shilingi bilioni 650 kwa Mwaka wa fedha 2021/2022 linafikiwa ifikapo mwezi Juni mwaka huu.

“Mikakati iliyowekwa ni pamoja na kuongeza maafisa  kwenye usimamizi wa shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini” amesema Dkt. Biteko.

Waziri Dkt. Biteko amewataka wachimbaji na wafanyabiashara wa madini nchini kuhakikisha wanaendesha shughuli zao kwa kufuata sheria na kanuni za madini na kusisitiza kuwa Serikali haitamwonea huruma mtu yeyote ayakayebainika anatorosha madini.

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Profesa Idris Kikula, amesema kuwa magari yatarahisisha kwa kiasi kikubwa utendaji kazi kwa kufika maeneo yasiyofikika kirahisi.

 
Picha ya magari saba ambayo yamekabidhiwa Tume ya Madini imeelezwa kuwa ni  moja ya mikakati ya kuboresha mazingira ya ukusanyaji wa maduhuli kwenye shughuli za uchimbaji na biashara ya madini nchini.
Waziri wa Madini, Dkt. Doto Biteko akikata utepe ishara ya kuzindua magari saba na kuyakabidhi Tume ya madini ikiwa ni moja ya mikakati ya kuboresha mazingira ya ukusanyaji wa maduhuli kwenye shughuli za uchimbaji na biashara ya madini nchini. Zoezi hilo limefanyika leo februari 21 mwaka huu kwenye ofisi za Wizara ya Madini Jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Madini, Dkt. Doto Biteko akizungumza na waandishi wa habari baada ya kukabidhi magari saba Tume ya Madini kama moja ya mikakati ya kuboresha mazingira ya ukusanyaji wa maduhuli kwenye shughuli za uchimbaji na biashara ya madini nchini.

No comments