BRELA YAJIPANGA KUSHIRIKI NANENANE MKOANI SIMIYU.
Na Noel Rukanuga, Dar es Salaam.
Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) imejipanga
kikamilifu kushiriki maonesho ya nanenane kwa kutoa huduma kwa washiriki
wanaotarajia kushiriki maonesho hayo ambayo yanatarajia kufanyika Mkoani Simiyu kuanzia Agosti 1-8 mwaka huu.
Akizungumza na waandishi wa
habari jijini Dar es Salaam Afisa Mtendaji Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) Emmanuel
Kakwezi, amesema
katika maonesho ya mwaka huu watatoa huduma pomoja na kuelimisha umma kuhusu
namna ya kusajili kampuni na majina ya biashara.
Bw. Kakwezi amesema kuwa ni vizuri wananchi kujitokeza ili waweze
kusajili biashara zao kwa urahisi katika msimu huu wa nanenane kwani
wamaejipanga kutoa huduma bora katika kuhakikisha kila mshiriki ananufaika na
huduma bora ya brela katika maonesho hayo.
“Brela
itakuwa inatoa huduma zake palepale viwanja vya simiyu, itakuwa inatoa huduma
zake zote ikiwamo kusajili makampuni, kusajili majina ya biashara, kutoa
leseni, kusajili alama za biashara kutoa hati na leseni za viwanda,” amesema
Bw. Kakwezi
Amesema kuwa lengo ni kuona shughuli uvuvi, kilimo na ufugaji haziishi
kukidhi haja ya matumizi ya nyumbani tu, zinatakiwa ziwe shughuli za kibiashara,huku
tukiendelea na utaratibu namna wanavyoweza kusajili makampuni na kuwasaidia
namna ya kupata masoko.
Mkurugenzi huyo ametoa wito kwa wananchi kutembelea banda la Brela kwa
sababu limesheheni wataalamu ambao watawasaidia kupata maelezo yanayohusu huduma zinazotolewa
na Brela pamoja na kupata elimu ya kurasimisha shughuli.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka, amesema kuwa Mhe.
Makamu wa Rais atafungua rasmi maonesho hayo Agosti Mosi mwaka huu na waoneshaji mbalimbali zikiwemo Taasisi,
Mashirika mbalimbali na wajasiriamali wataanza kuonesha teknolojia, huduma na
bidhaa zao Julai 29 mwaka huu.
“Shughuli ya ufunguzi itafanywa tarehe 01/08/2019 na Mhe.
Makamu wa Rai, haya ni maonesho ambayo yatakaribisha viongozi wa Kitaifa,
Agosti 03, 2019 tutakuwa na Mhe. Waziri Mkuu, Agosti 06, 2019 tutakuwa na
Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Pinda na Kilele tunatarajia kuwa na Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli” amesema.
RC Mtaka amesema katika maonesho
hayo wanatarajia kuwashirikisha watu zaidi ya elfu 50 ambapo pia
yatawashirikisha maofisa mbalimbali wa Serikali ambao watakuwa na shughuli za
kuwasaidia wananchi huku akiwataka wakulima na wajasiriamali kujitokeza kwa
wingi katika maonesho haya.
Maonesho ya nanenane Kitaifa yanafanyika kwa mara ya
pili mkoani Simiyu tangu Kanda ya Ziwa ilipogawanywa katika kanda mbili ambapo
mwaka huu yanaadhimishwa chini ya kauli Mbiu:-“KILIMO, MIFUGO NA UVUVI KATIKA
UKUAJI WA UCHUMI WA NCHI”.
Post a Comment