Ads

Benki ya Amana na TY Services Limited zaingia mkataba kuwawezesha madereva kumiliki vyombo vya moto




Hussein Ndubikile
Mwamba wa Habari
Benki ya Amana na Kampuni ya TY Services Limited inayoendesha mtandao wa Taxify nchini zimesaini mkataba wa kuwawezesha madereva  wa mtandao huo  kumiliki vyombo vya moto.
Akizungumza na wanahabari wakati wa utiaji saini mkataba huo leo jijini Dar es Salaam Meneja Mkuu wa Kitengo cha Biashara cha benki hiyo, Dassu Mussa amesema Benki ya Amana inaendeshwa kwa kuzingatia misingi ya kiislam hivyo uingiaji mkataba huo  ni sehemu ya mikakati ya kuifanya kuwa benki kiongozi katika kutoa huduma  za kibunifu zenye lengo la kuinua jamii kiuchumi.
“ Uwezeshaji utafanyika katika vikundi, hivyo madereva  watahaitajika kuunda kikundi cha madereva 10 ambao watadhaminiana wenyewe,” amesema.
Amebainisha kuwa dereva atatakiwa kuweka amana isiyopungua asilimia 10 ya thamani ya chombo cha moto anachohitaji  kuwezeshwa na kwamba amana hiyo itatumika kama dhamana mpaka dereva atakapokamilisha marejesho.
Amesisisitiza kuwa dereva wa mtandao huo atatakiwa kuweka akiba ya Sh 15000 kila wiki ambayo itakuwa kama dhamana hadi mwisho wa marejesho.
Amefafanua kuwa dereva atafanya marejeshon kulingana na makubaliano na benki hiyo katika kipindi kisichopungua miaka miwili huku akibainisha watazingatia vigezo mbalimbali katika kutoa uwezeshaji ikiwemo dereva kuwa na uzoefu wa kutosha na rekodi nzuri.
Kwa upande wake Meneja wa Mtandao wa Taxify nchini, Remmy Eseko amesema mkataba walioingia ni moja ya mikakati ya kuhakikisha wanatoa huduma ya usafiri kwa gharama nafuu na kuwaongezea madereva kipato.
Amewahaimiza madereva wanaotumia mtandao huo kuchangamkia fursa hiyo yenye lengo la kuhakikisha wanamiliki vyombo vyao vya moto kupitia benki hiyo.
Aidha, amesema anaamini mtandao huo utatoa huduma bora kwa wale wote watakaotumia.

No comments