Ads

DKT. NDUGULILE AING’ARISHA PROGRAMU YA KIKUNDI MLEZI KWA WANAWAKE WAJASIRIAMALI MKOANI KATAVI.


Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile (Mb) akiangalia moja ya bidhaa ya mvinyo inayotengenezwa na Kikundi cha Wanawake wajasiriamali cha Humbaji kilichopo katika Manispaa ya Mpanda alipofanya ziara ya siku mbili ya kuamsaha ari ya wananchi kufanya shughuli za maendeleo ili kuchangia azma ya kufikia uchumi wa kati na wa viwanda.

Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile (Mb) ameing’arisha programu ya ‘Kikundi Mlezi’ katika Manispaa ya Mpanda mkoani Katavi yenye lengo la kuwawezesha wanawake wajasirimali kuwezeshana  wenyewe katika kuanzisha na kuendeleza miradi ya biashara zao.

Dkt. Ndugulile ameitambulisha  programu hiyo wakati alipofanya ziara ya siku mbili katika manispaa ya Mpanda mkoani Katavi katika zoezi la kuamsha ari ya wananchi kuibua miradi na kuanzisha shughiuli za uzalishaji kawa kuzingatia fursa, mazingira na soko.

Dkt.Ndugulile amesema kuwa  ili kufanikisha kufikiwa kwa Tanzania ya viwanda Serikali itaendelea kuwasaidia wajasiriamali wadogo wadogo hasa wanawake katika kuwawezesha kuanzisha vikundi vitakayoanzisha viwanda vidogo vidogo na vya kati.

Ameongeza kuwa lengo la kuzindua Programu ya ‘Kikundi Mlezi’ ni kuwashirikisha wanawake wajasirimali waliokomaa katika biashara kuwasaidia wanawake wajasiriamali wanaoanza shughuli hizo kwa kuwapatia uelewa wa soko, mbinu za biashara, upatikanaji wa mikopo na mahitaji ya kiufundi.

“Niseme programu hii itasaidia kwa asilimia kubwa kuibua wanawake ambao hawakuwa na uwezo katika kuanzisha biashara zao na kufanya wanawake kujiunga na vikundi na hatimaye kuanzisha viwanda vidogo na vya kati”alisisitiza Mhe. Dkt. Ndugulile.

Kwa upande wake Mkuu wa  Wilaya ya Mpanda Mhe. Lilian Matinga amesema kuwa program ya ‘Kikundi Mlezi’ itasaidia kuwainua wanawake na kujitokeza kwa wingi kujishughulisha na shughuli za uzalishaji.

Naye Mwakilishi wa Katibu Mkuu Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto Bw. Julius Mbilinyi  amesema kuwa Wizara itaendelea kuhamasisha wanawake kujitokeza na kujiunga na vikundi na kusaidiana katika kuendesha biashara ambazo zitawasaidia kujikwamua kiuchumi.

Mmoja wa Wanawake wajasiliamali Wilayani Mpanda Bi.Nuru Saimon ameishukuru Serikali kwa kuzindua Mpango huo utakaowawezesha wanawake kusaidiana  katika kuanzisha na kuinuka katika biashara ambazo zitawasaidia kujikwamua kiuchumi.

Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile (Mb) amefanya ziara ya siku mbili mkoani Katavi na kuwatembelea wanawake wajasiliamali katika kuhamasisha wanawake kujishughulisha ili kusaidia kufikia lengo la kuwa na Tanzania ya Viwanda. Msisitizo umetolewa kwa wananchi kupenda bidhaa zetu kwa kununua bidhaa zetu wenyewe ili kufikia lengo la uanzishaji wa viwanda 100 kwa kila mkoa.

No comments