Ads

TMA YAUNGANA NA NCHI NYENGINE WANACHAMA WA WMO KUADHIMISHA SIKU YA HALI YA HEWA DUNIANI.


Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuz i- Sekta ya Uchukuzi Mhe. Atupele Mwakibete akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Siku ya Hali ya Hewa Duniani.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Ladislaus Chang'a akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Siku ya Hali ya Hewa Duniani.

.........

Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuz i- Sekta ya Uchukuzi Mhe. Atupele Mwakibete amewataka wadau mbalimbali nchini nchini kutumia  vyema taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kwa ajili ya kupanga shughuli za kijamii na kiuchumi na kufanya maamuzi pamoja na kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.

Akizungumza na waandishi wa habari  leo Machi 23, 2023 kuhusu siku ya Kimataifa ya Hali ya Hewa Duniani, Mhe. Mwakibete, amesema kuwa  Tanzania ni miongoni mwa nchi 193 wanachama wa WMO na imeungana na Jumuiya ya Kimataifa kuadhimisha miaka 73 ya WMO na maadhimisho ya miaka 150 ya Shirika la Kwanza la Kimataifa la Hali ya Hewa.

"Uchumi wa Tanzania, unategemea sana sekta zinazotegemeana na zinazoathiriwa na hali ya hewa na upatikanaji wa rasilimali maji ambazo ni muhimu katika kupanga na kufanya maamuzi ambapo miongoni mwa sekta hizo ni kilimo, mifugo, uvuvi, nishati na maji, pia mfumo na mzunguko wa maji huchangia kutengeneza mvua ambayo tunategemea katika upatikanaji wa rasilimali maji," amesema Mhe. Mwakibete

Amesema kuwa kuwa utoaji wa huduma bora za hali ya hewa na maji umekuwa kipaumbele kwa Serikali ya Tanzania katika awamu zote, huku akieleza kuwa huduma hizi zina umuhimu mkubwa na kuongeza tija katika maendeleo ya sekta zote za kijamii na kiuchumi.

Amesema kuwa katika kuhakikisha kunakuwa na taarifa za uhakika za hali ya hewa, serikali ya Tanzania imefanya uwekezaji katika huduma za hali ya hewa ikiwemo ununuzi wa miundombinu ya kisasa ya uchunguzi wa hali ya hewa ikiwa ni pamoja na Rada za hali ya hewa.

"Kuna rada saba ambapo rada tatu zimeshasimikwa katika maeneo tofauti tofauti ya nchi, rada mbili zimeshafika na zinategemea kufungwa hivi karibuni katika Mkoa wa Mbeya na maeneo ya Kigoma na rada zingine mbili zipo kiwandani zinatengenezwa," amesema Mhe.Mwakibete

Ameongeza kuwa serikali ya Tanzania itaendelea kushughulikia mapungufu na mahitaji yanayohusu utoaji huduma za hali ya hewa nchini kwa nia ya kuboresha huduma za tahadhari zinazoendana na kasi na kukabiliana na maendeleo ya kimataifa ya sayansi na teknolojia. 

Ameeleza kuwa serikali inaunga mkono Mpango wa Umoja wa Mataifa wa kuhakikisha kuwa tahadhari za hali ya hewa zinawafikia watu wote duniani.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa, Dkt. Ladislaus Chang'a amesema kuwa Shirika la Hali ya Hewa Duniani linataka taasisi zote zinazotoa utabiri walau usahihi uwe asilimia 70.

Amesema kuwa  kwa Tanzania usahihi mpaka sasa utabiri ni asilimia zaidi ya 86 ni nchi ambayo inaheshimika kwa ubora wa utabiri na huduma za hali ya hewa duniani.

"Katika Afrika, serikali ambazo zimewekeza katika kuimarisha huduma za hali ya hewa, Tanzania ni namba moja na hii ni kutokana uwekezezaji mkubwa na uwezesheja tunaopatiwa na serikali yetu na kwa sasa tuna rada saba ambapo zote zikifungwa tutakuwa tumekidhi mahitaji yetu," amesema Dkt.Chang'a

Hata hivyo Dkt.Chang'a amebainisha kuwa mvu zinazoendelea zinatarajia  kuwa za wastani katika maeneo mengi, hivyo inawasisitiza wakulima kuzingatia ushauri wa kitaalam kutoka kwa Maafisa Ugani ambao wanaweza kutafsiri vizuri taarifa hizo pamoja na kupanda mazao yanayokomaa haraka na yanayostahimili hali ya ukame.

Kauli mbiu ya Siku ya Hali ya Hewa Duniani kwa mwaka huu ni "Ustakabali wa Hali ya Hewa, Tabianchi na Maji kwa Vizazi Vyote".

Maadhimisho ya Mwaka huu  yanaangazia mustakabali wa huduma hizo kwa vizazi vyote, upimaji na ubadilishanaji wa taarifa au data na utaalamu kwa lengo la kukuza ushiriki wa wanasayansi watoa maamuzi na vijana katika uzalishaji na matumizi ya taarifa za hali ya hewa na rasilimali za maji.

No comments