Ads

SERIKALI KUWABANA WAMILIKI WA VYOMBO VYA USAFIRISHAJI WATAKAOKAIDI KUTOA MIKATABA KWA MADEREVA.

 


Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu. Mhe. Patrobas Katambi akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo tarehe 22/7/2022 kuhusu hatua zilizochukuliwa na serikali katika hoja na malalamiko yaliyowasilishwa na wafanyakazi madereva na wamiliki wa vyombo vya usafirishaji.

NA NOEL RUKANUGA, DAR ES SALAAM

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesema itaanza kuwachukulia hatua waajiri na wamiliki vyombo vya Usafirishaji nchini ambao watabainika kukaidi maelekezo ya kisheria (Compliance Order) ya kutoa mikataba kwa wafanyakazi madereva ifikapo mwishoni mwa mwezi Agosti, 2022.

 

Hatua hiyo imekuja baada serikali kufanya ukaguzi katika Mikoa ya Dar es salaam, Arusha, Mwanza, Pwani na Mbeya ambapo imebainika jumla ya Kampuni 73 zilikaguliwa na kubaini baadhi ya waajiri hawajatoa mikataba kwa Madereva.

 

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo tarehe 22/7/2022 na waandishi wa habari, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu. Mhe. Patrobas Katambi, amesema kuwa kuhusu mishahara ya madereva kupitia benki, sheria ya ajira na mahusiano kazini, sura 366 imeruhusu mwajiri na mfanyakazi kukubaliana namna ya kulipana mshahara ama kupitia benki, fedha taslim au hundi.

 

Serikali inawashauri madereva kufanya makubaliano na waajiri wao kuhusu suala hilo. aidha, kupitia kaguzi zinazoendea kufanyika katika maeneo ya kazi, serikali itasimamia suala la madereva kupatiwa hati za malipo ya mshahara (salary slip) kama inavyoelekezwa kwenye sharia” amesema Mhe. Katambi.

Amesema kuwa kuhusu bima ya Afya, NSSF na Pensheni kwa Wastaafu, suala hilo lipo kwa mujibu wa sheria ambayo inawataka waajiri wote kuwasajili na kuwachangia wafanyakazi wao katika Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (NSSF na WCF) wakiwemo wafanyakazi madereva.

Ameeleza kuwa katika ukaguzi uliofanyika awali ilibainika kuwa baadhi ya waajiri hawajawasajili madereva wao katika mifuko hiyo, hivyo maelekezo ya kisheria yametolewa na serikali itaendelea kufuatilia waajiri hao ili kuhakikisha wanatekeleza.

Mhe. Katambi amefafanua kuwa kuhusu suala la matumizi ya Vidhibiti mwendo (Speed Governor) badala ya VTS; matumizi ya vidhibiti mwendo yapo kwa mujibu wa sheria ya usalama barabarani sura 168 iliyofanyiwa marejeo mwaka 2002.

 

“Katika kutekeleza Sheria hiyo, wamiliki wote wa mabasi wameelekezwa kufunga vidhibiti mwendo kwenye mabasi yao ndani ya miezi 6 (kufikia Septemba, 2022). Serikali inatambua VTS kama kifaa halali cha kufuatilia mwenendo wa mabasi, hivyo, Speed Governor na VTS vitaendelea kutumika kudhibiti mwendo” amesema Mhe. Katambi.

 

Katika hatua nyengine amebainisha kuwa serikali imetoa mwongozo wa kupakia na kushusha mafuta wa mwaka 2021 kwa wadau wote wa usafirishaji wa mafuta (bohari za mafuta, wamiliki wa vituo vya mafuta, madereva na wasafirishaji wa mafuta).

 

Amesema kuwa  ni jukumu la kila mdau kuhakikisha taratibu za upakiaji mafuta zinafuatwa wakati akiwa katika bohari yoyote na  serikali itaendelea kutoa elimu kwa wadau wote ili waweze kuzingatia mwongozo huu na hatua za kisheria zitachukuliwa kwa wadau watakaokiuka.

Utaratibu wa kusafirisha sumu, suala hili lipo kwa mujibu wa Sheria ya Kemikali za Viwandani na Majumbani Sura 182 ambayo imetoa mamlaka kwa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali kusimamia wasafirishaji kwa kuwasajili wamiliki wa vyombo vya usafirishaji na kutoa mafunzo kwa Madereva wanaosafirisha sumu ndani na nje ya nchi.

Aidha, kwa mujibu wa utaratibu imekubalika kuwa Vyeti anavyopatiwa Dereva baada ya kupatiwa mafunzo kwa ufadhili wa Mwajini na Mali ya Dereva.

Hivyo, ili kuhakikisha madereva hawalazimiki kupatiwa mafunzo wakiwa kazini,Serikali inaendelea na hatua za kujumuisha mafunzo ya kusafirisha mafuta na kemikali hatarishi katika mtaala wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) ili kuwezesha kila Dereva anayehitimu kuwana uelewa wa namna bora ya kusafirisha mafuta na kemikali hatarishi.

Kuhusu ubovu wa magari, Serikali imetoa maelekezo kwa Wakuu wa Vikosi vya Usalama Barabarani wa Mikoa (RTOs) kufanya ukaguzi wa magari na kuchukua hatua kwa mujibu wa Sheria.

 Aidha, Serikali kupitia Jeshi la Polisi na LATRA inafanya jitihada za kuwa na Mfumo wa Ukaguzi wa lazima wa magari (Mandatory Vehicle Inspection) ambao unatumia mitambo ya kisasa.

 

Kuhusu kuanzisha Kanzi Data ya Madereva; Sheria ya LATRA Namba 9 ya mwaka 2019 imeipa jukumu Mamlaka kuwathibitisha Madaereva. Katika kutekeleza hilo, LATRA imetengeneza Mfumo (Kanzi Data) ambao unawasajili Madereva wote wa magari ya biashara.

 

Hadi kufikia Juni, 2022, LATRA imesajili zaidi ya Madereva 10,236. Serikali inasisitiza Madereva waendelee kujisajili kwenye Mfumo huo ili kukidhi matakwa ya Sheria.

 

Kuhusu hoja ya kuitisha vikao vya mashauriano ya wadau, Serikali imepokea hoja hiyo na tayari imetekelezwa kwa kuitisha vikao vinavyoendelea. Aidha, itaendelea kuitisha vikao hivyo kama sehemu ya utekelezaji wa majukumu ya kawaida bila kusubiri kuibuka kwa migogoro.  

 

Kuhusu suala la Madereva kujiunga na vyama vya wafanyakazi. Suala la kujiunga na vyama vya wafanyakazi ni la hiari kwa wafanyakazi.

 

Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Sura 366 inakataza waajiri kuwazuia wafanyakazi kujiunga na vyama husika. Serikali itaendelea kutoa elimu kwa Madereva na wamiliki wa Vyombo vya Usafirishaji kuhusu umuhimu wa wafanyakazi kujiunga na vyama na kuchukua hatua kwa waajiri watakaozuia Madereva kujiunga na vyama hivyo.

 

Kuhusu mabasi ya abiria kuingia kila kituo kwa safari za mikoani. Serikali imeondoa vituo vilivyokuwa vinalalamikiwa ambapo kwa sasa magari hayalazimiki kuingia katika kila kituo, badala yake mabasi yataingia katika vituo vikuu. LATRA imeshatoa ratiba mpya kutekeleza suala hili.

 

Kuhusu Maafisa Rasilimali watu na Maafisa Mahusiano kutotimiza wajibu wao, Kupitia kaguzi zinazoendelea kufanyika katika maeneo ya kazi, elimu inaendelea kutolewa kwa Maafisa husika ili kukuza uelewa wao katika kusimamia rasilimaliwatu.

 

Pamoja na hatua zilizochukuliwa, ninawasihi Viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi wazingatie utaratibu uliowekwa kisheria katika majadiliano ya kutetea maslahi ya wafanyakazi na kutatua migogoro ya kikazi.

 

Aidha, nitoe rai kwa Madereva wasio wanachama wa Vyama vya Wafanyakazi kuacha kutumia njia zisizo halali kisheria kuanzisha au kuchochea vurugu na migomo.

 

Vilevile, nitumie fursa hii tena kutoa maelekezo kwa waajiri wote nchini kutekelezeza Sheria za Kazi na maagizo niliyoyatoa ikiwa ni pamoja na kutoa mikataba ya kazi ili kujenga mahusiano mema sehemu za kazi.

 

Madereva na Wamiliki wa Vyombo vya Usafirishaji, serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, itaendelea kushirikiana nanyi kwa kuhakikisha kero na changamoto zinazoikabili sekta hii zinapatiwa ufumbuzi wa kudumu amesema Mhe. Katambi.

 

Serikali inatambua kwamba, kutozipatia ufumbuzi kero na changamoto katika sekta hii ni kurudisha nyuma jitihada zinazoendelea kufanywa na Serikali yetu katika kuhakikisha inaimarisha miundombinu ya usafirishaji nchini na kuvutia uwekezaji na mazingira bora ya biashara.

No comments