Ads

Manispaa ya Ilala yatekeleza Miradi ya Maendeleo mwaka 2018/19 kwa asilimia 78



 Image result for picha madiwani ilalal
Mwamba wa habari
Halmashauri ya Manispaa ya Ilala imesema kuwa katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2018/19 imefanikiwa kutekeleza Miradi ya Maendeleo kwa asilimia 78 huku ikibainisha kutenga Sh bilioni 21.3 na kwamba kati ya hizo Sh bilioni 17.2 zimetumika katika kutekeleza miradi hiyo.

Hayo yalibainishwa  jijini Dar es Salaam na Mchumi wa manispaa hiyo, Ando Mwankuga katika Kikao cha Kawaida cha Baraza la Madiwani wa Manispaa hiyo kilichopitia na kuangalia utekelezaji wa miradi hiyo katika kipindi cha mwaka mzima.
Alisema katika kipindi cha fedha cha mwaka huo manispaa ilitenga Sh bilioni 56.2 lakini ilivuka malengo kwa kukusanya Sh bilioni 58 sawa na asilimia 102  hali iliyochangia kufanikisha miradi hiyo kupata fedha ya kutosha.

 Alibainisha kuwa  katika kipindi hicho cha bajeti manispaa ilitenga Sh bilioni 21.3 huku ikitumia Sh bilioni 17.2 kukamilisha miradi ya ujenzi wa madarasa ya shule za msingi, sekondari na vituo vya afya.

" Miradi ya elimu na afya imetekelezwa ndani ya kipindi hicho ujenzi wa madarasa umesaidia wanafunzi wote wa darasa la saba waliomaliza mwaka jana kujiunga kidato cha kwanza," alisema Mwankuga.

Alisisitiza kuwa kiwango hicho cha fedha kimefanikisha Ujenzi wa miradi ya madarasa ya shule za msingi na sekondari pamoja na vituo vya afya kikiwemo Kituo cha Magonjwa ya Kuambukiza kilichopo Kipawa.

Pia alisema mafanikio ya utekelezaji miradi hiyo umechangiwa na utendaji kazi madhubuti wa Mkurugenzi wa manispaa hiyo, Jumanne Shauri pamoja na ushirikiano kutoka kwa madiwani.

Katika hatua nyingine, Mwankuga alisema manispaa hiyo imefanikiwa kutekeleza kwa asilimia 100 Ilani ya Serikali ya Awamu ya Tano inayozitaka halmashauri zote kutenga asilimia 10 ya mapato kwa ajili ya mikopo ya vikundi vya Vijana, wanawake na walemavu ambapo Sh bilioni 3.7 zimwetolewa.

Wakati huo huo, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoa wa Ilala imeomba kutoa elimu ya rushwa kwa madiwani wa baraza hilo ili kuwasaidia kutoa elimu kwa jamii wanayoiongoza.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudhibiti Ukimwi wa baraza hilo ambaye pia ni Naibu Meya wa Manispaa hiyo, Douglas Massaburi alisema katika kipindi cha mwaka 2018/19 watu 55,695 wamepatiwa huduma ya upimaji ya Virus vya Ukimwi huku akibainisha vifo 91 vimetokea.

No comments