Ads

NEMC IMULIKE UTEKELEZAJI WA SHERIA YA MAZINGIRA MIRADI YA UWEKEZAJI

Image result for picha ya makamba

Na Ismail Ngayonga
MAELEZO


SEKTA zote za uzalishaji mali ikiwemo kilimo, maji na nishati zinategemea mazingira kama rasilimali muhimu katika kuchangia ukuaji wa uchumi wa nchi.
Hata hivyo, shughuli zisizo endelevu za uzalishaji mali ikiwemo ukataji holela wa miti, uvuvi haramu, uzalishaji na utupaji holela wa taka zimechangia kwa kiasi kikubwa katika uharibifu wa ardhi, ukosefu wa maji safi na salama kwa wananchi, pamoja na upotevu wa bioanuai na makazi.
Maendeleo endelevu hayawezi kupatikana bila kutunza mazingira, ingawa jitihada  kubwa za utunzaji wa mazingira zimefanyika hali ya mazingira nchini bado si ya kuridhisha na imekuwa tishio kwa mustakabali wa Taifa letu.
Shughuli ya uhifadhi wa mazingira inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo teknolojia ya uhandisi jeni, viumbe wageni/vamizi, biofueli, na taka za  kielektroniki, pamoja na ukosefu wa wataalam wa kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, Sura 191 katika ngazi zote.
Kutokana na Tanzania kukabiliwa na tishio la kuenea kwa hali ya jangwa na ukame, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) inaratibu maandalizi ya Programu ya Kitaifa yenye madhumuni ya kufanya tathmini ya maeneo yaliyoathirika ili kuweka malengo ya kuzuia uharibifu wa ardhi ifikapo mwaka 2030.
Akiwasilisha Hotuba ya Makadirio ya Bajeti ya mwaka 2018/19, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, January Makamba anasema Ofisi yake kupitia Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Iimeendelea kusimamia na kutekeleza shughuli za uzingatiaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, Sura 191 na Kanuni zake.
Makamba anasema NEMC imekuwa likishiriki katika hatua zote muhimu za utekelezaji wa miradi mikubwa ya kitaifa kama vile, mradi wa kufua umeme wa Stiegler’s Gorge na mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi na kushirikiana na wawekezaji katika sekta muhimu za kiuchumi ili kuhakikisha kuwa miradi yao inafuatiliwa kwa karibu na kupata hati kwa muda mfupi.
Anaongeza kuwa katika mwaka 2017/18, NEMC ilifanya ukaguzi na ufuatiliaji wa miradi 627 katika mikoa 23 nchini ikiwemo Arusha, Kilimanjaro, Manyara, Pwani, Morogoro, Kigoma, Tabora, Dar es Salaam, Tanga.
Anaitaja mikoa mingine kuwa ni pamoja na Geita, Mwanza, Dodoma, Songwe, Iringa, Lindi, Kagera, Mbeya, Ruvuma, Singida, Mara, Shinyanga, Simiyu na Mtwara, ambapo NEMC imeshughulikia malalamiko 207 ya uchafuzi na uharibifu wa mazingira kutoka kwa wananchi.
Waziri Makamba anasema katika kipindi cha mwaka 2017/18, Baraza kwa kushirikiana na Chuo cha Madini na Halmashauri za Wilaya husika katika mikoa ya Geita na Shinyanga limefanya tathmini kwa wachimbaji wadogo wa dhahabu ili kuhakiki iwapo wanazingatia Sheria na Kanuni zake.
Tathmini hii ilihusisha wachimbaji wadogo wanaotumia Zebaki na wachenjuaji wanaotumia Sayanaidi (Cyanide) na katika mwaka 2018/19, Baraza litaendelea litaendelea kutoa elimu kwa wachimbaji wadogo na kufanya ufuatiliaji wa mara kwa mara ili kutatua changamoto zilizobainika katika tathmini hiyo” anasema Waziri Makamba.
Anaongeza kuwa katika kuimarisha uzingatiaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, Ofisi yake imeteua wakaguzi 512 kutoka katika taasisi za Umma na Serikali za Mitaa pamoja na kutoa mafunzo kwa wakaguzi wa mazingira 128 kwa ajili ya kuongeza  uwezo  wa  Serikali   kusimamia   hifadhi   ya mazingira.
Kwa mujibu wa Waziri Makamba anasema NEMC limesimamia uteketezaji wa taka hatarishi kutoka katika Vyuo Vikuu, Viwanda, Magereza, Migodi, Viwanja vya Ndege na Maduka ya Madawa, ambapo imeteketeza madawa chakavu yenye uzito wa tani 244.617 na lita 97 kwenye  mtambo  wa  Tindwa  Incinerator,  Mgodi wa Buzwagi, Hospitali ya Muhimbili (Kampasi ya Mloganzila) na Safe Waste Incinerator ya Mkuranga.
Kuhusu Tathmini ya Athari za Mazingira (TAM), anasema katika mwaka 2017/18 Baraza limesajili jumla ya miradi 1,176 kwa  ajili  ya  kufanyiwa  mchakato  wa  kupata  hati  za TAM na miradi 533 imepewa vyeti kati ya miradi iliyosajiliwa.
Hadi kufikia Desemba 2017, NEMC imesajili wataalamu elekezi wa TAM 757, Wakaguzi wa Mazingira 357, Kampuni za Ushauri wa TAM 152 na za Ukaguzi wa Mazingira 74 na kukamilisha maandalizi ya Mfumo wa kuchakata TAM kwa njia ya mtandao” Anasema Waziri Makamba.
Waziri Makamba anasema kutokana na na malalamiko ya wawekezaji kucheleweshewa kupata cheti cha TAM, NEMC imechukua hatua mbalimbali ikiwemo Kupunguza gharama za TAM, Kutoa vibali vya muda (kwa miradi ya viwanda pamoja na Kutengeneza orodha ya mambo muhimu ya kuzingatia ya miradi ya majengo chini ya ghorofa tatu, viwanda na umeme jua.


Usimamizi wa Sheria ya Mazingira, Sura Na. 191 inapaswa kutekelezwa ili kuweka mtazamo mpya katika namna bora ya kuchakata taka ikiwemo   ukusanyaji na usafirishaji wa taka na kuzitumia kama malighafi ya kutengenezea mbolea, uzalishaji wa nishati ya umeme na utengenezaji wa madampo ya kisasa.

No comments