TUCHANGAMKIENI FURSA DUNIANI KOTE: RAIS MAGUFULI
Na. Immaculate Makilika
mwambawahabari
Watanzania wametakiwa kujishughulisha katika shughuli za kujiletea maendeleo kwa kutumi fursa zinazopatikana katika maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi ili kujikwamua kiuchumi.
Akizungumza na wahariri pamoja na waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari leo, Ikulu jijini Dar es Salaam Rais Magufuli alisema kuwa watanzania wanakila sababu ya kujipatia maendeleo kwa vile wamezungukwa na fursa mbalimbali ikiwemo kuwa mwananchama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) pamoja na Jumuiya ya Nchi za Afrika Mashariki (EAC) ambapo wanaweza kutumia fursa hiyo ili kujiletea maendeleo.
“Wito wangu kwa watanzania ni huu tuchangamkieni fursa duniani kote, kwa vile watanzania tuna uwezo wa kuzungumza lugha ya Kiswahili kwa ufasaha, tumesoma vizuri na tunaweza kufanya ujasiriamali, hivyo tunaweza kutumia fursa zilizopo katika soko la jumuiya ya SADC yenye nchi 15 na nchi 6 za jumuiya ya EAC” alisema Rais Magufuli
Mbali na hayo, Rais Magufuli amezungumzia masuala mbalimbali ikiwemo fursa za uwekezaji kwa watanzania wanaoishi ughaibuni (diaspora) ambapo amewataka kuja nchini kwa ajili ya kuwekeza kwa vile serikali imejiandaa kuhakikisha kunakuwepo na mazingira yanayovutia wawekezaji nchini.
“Tunawakaribisha wageni kutoka nchi mbalimbali duniani kuja kuwekeza, kwa hiyo hata watanzania wanaoishi nje ya nchi tunawakaribisha kuja kuwekeza katika maeneo mbalimbali ya uzalishaji” alisema Rais Magufuli
Aidha, Rais Magufuli amewataka wahariri pamoja na waandishi wa habari kutumia taaluma yao katika kuleta chachu ya maendeleo kwa kuandika na kutangaza habari zenye kumjenga mtanzania na kusisitiza kuwa wazalendo pamoja na kuweka mbele maslahi ya Taifa kwa faida ya kizazi cha sasa na cha baadae.
Post a Comment