Ads

“SHERIA YA MUSWADA WA HUDUMA ZA HABARI IMECHELEWA” RAIS MAGUFULI


Inaonyesha 1.jpg
Na. Immaculate Makilika 
  mwambawahabari

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John  Magufuli amesema kuwa huu ni wakati mwafaka kwa muswada wa sheria ya huduma  za vyombo vya habari  kukubaliwa na kuwa sheria kwa vile tasnia ya habari inakumbwa na changamoto nyingi  zitakazotatuliwa na sheria hiyo.

Akizungumza na wahariri pamoja na waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari leo, Ikulu jijini Dar es Salaam Rais Magufuli alisema kuwa muswada huo ni wa muda mrefu na sasa ni wakati mwafaka kwa vile tansia ya habari inakumbwa na changamoto nyingi zinazoweza kutatuliwa  na  muswada huo.


“Hii sheria ya huduma za vyombo vya habari imechelewa  kwa vile mchakato wake ulianza tangu mwaka 2011 hadi sasa mwaka 2016 wadau walikuwa na muda wa kutosha wa kujiandaa na kutoa maoni yao ambayo yangeweza kuboresha muswada huo” alisema Rais Magufuli

Ameongeza kuwa, Sheria hii italeta mabadiliko katika tasnia ya habari kwa vile kutakuwepo na Bodi ambayo itashughulikia masuala ya taaluma ya habari, pamoja na mambo mengine yaliyoanishwa katika muswada huo ambayo ni maslahi ya waandishi wa habari nchini.

Muswada huu unatazamiwa   kuwajengea uwezo waandishi wa habari ili waweze kufanyakazi kitaalamu  kwa kuandika  na kutangaza habari zenye ukweli zitakazochangia katika harakati za kuleta   maendeleo kwa  nia ya kuwasaidia watanzania na serikali kwa ujumla katika  kufikia malengo yake.

Muswada wa Sheria ya huduma za habari umesomwa  leo Novemba 4,  2016 katika kikao cha  tano cha Bunge na mkutano wa 11, ambapo utajadiliwa na kufuata taratibu zingine kabla ya kuwa sheria.

No comments