Watanzania watakiwa kuongeza thamani na uzalishaji katika sekta ya viwanda nchini.
Na. Eliphace Marwa
Mwambawahabari
Watanzania watakiwa kuongeza thamani na uzalishaji katika sekta ya viwanda nchini.
WAZIRI wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage amewataka watanzania kuongeza thamani ya bidhaa na uzalishaji ili kuongeza fursa za ajira.
Mwijage ameyasema hayo wakati akizungumza na wawakilishi wa mashirika ya kiserikali na makampuni binafsi wakati wa sherehe za utoaji tuzo za pili za KAIZEN zinazoratibiwa na Shirika la uhusiano wa kimataifa laJapan (JICA).
“Tuko hapa hii leo kushuhudia sherehe za utoaji wa tuzo katika sekta ya viwanda ambayo ni matunda ya dhana za KAIZEN kwani tuzo hizi zinatolewa kwa makampuni yaliyofanya vizuri katika kutekeleza mbinu za KAIZEN ili kuweza kutoa changamoto kwa makampuni mengine” alisema Mh. Mwijage
Kwa upande wake Mwakilishi Mkuu wa JICA ofisi ya Tanzania Bw. Toshio Nagase aliipongeza Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji pamoja na kitengo cha KAIZEN Tanzania kwa kuandaa sherehe yenye mafanikio kwa mara nyingine kufuatia ili iliyofanyika mwaka jana.
“Baada ya uzinduzi wa mpango wa miaka mitano, sisi sote tumetambua umuhimu wa kukuza viwanda ili kufikia maendeleo ya kiuchumi na kijamii hapa Tanzania”, alisema Bw. Toshio
Aidha Bw. Toshio alibainisha baadhi ya maeneo ambayo KAIZEN imefanikiwa kuwa ni pamoja na kuhakikisha ubora wa bidhaa na kubadilisha tabia pamoja na kutoa motisha kwa wafanyakazi.
Kwa upande wake Mwakilishi wa KAIZEN Tanzania Bw. Takao Kikuchi amesema kuwa anaamini kuitangaza KAIZEN nchini Tanzania ni jambo la muhimu ili kutengeneza viwanda vyenye ushindani na kufanikisha lengo la kukuza viwanda kuelekea mwaka 2025.

Post a Comment