Ads

WAZEE ACT WAZALENDO WASISITIZWA UMUHIMU WA UMOJA NDANI YA CHAMA

NA FRANCIS PETER.

Wazee wa Chama cha ACT Wazalendo wametakiwa kuwa na umoja na mshikamano ndani ya chama na jamii katika utekelezaji wa majukumu yao jambo ambalo litasaidia kutetea maslahi mapana ya Taifa.


Akizungumza leo Mach 1, 2024 Jijini Dar es Salam na Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Prof. Azaveri Lwaitama wakati akifungua mkutano mkuu wa Ngome ya Wazee wa Chama hicho ambao umeenda sambamba na kuchagua viongozi wa nafasi mbalimbali katika ngome hiyo.

Amesema kuwa, ni vyema wajumbe wa mkutano huo kuchagua viongozi ambao wanauwezo wa kuongoza na kuacha tabia ya kuchagua viongozi kwa mfumo kwani matokeo yake wanakosekana viongozi bora wanaoweza kuongoza katika misingi inayotakiwa kwa busara na hekima.

“Mukitaka kufika mbali lazima muwe na sauti ya pamoja hata kama munatofautiana kwa itikadi ya vyama vyenu lakini linapokuja suala la kutetea maslahi ya nchi lazima mushikamane, hamuwezi kuondoa chama kilicho madarakani kwa kujitenga “amesema Prof Lwaitama.

Akitoa salamu fupi katika mkutano huo, Kamishna Msaidizi Mstaafu wa Jeshi la Polisi SACP Jamal Rwambo amesema kuwa mfumo katika vyama vya siasa ni tatizo sana, hivyo kama upo katika chama cha Act Wazalendo wanachama wanatakiwa kuukataa kwa vitendo kwani unakwamisha sana kupata viongozi bora ndani ya chama.

“Mfumo wa rushwa unawaweka pembeni watu ambao wangeweza kulisaidia taifa kwa uongozi wao, wachagueni watu wenye sifa kiongozi mzuri anaeweza kuisaidia ngome ya wazee ni yule ambae ni mkweli na sio muongo”amesema SACP Jamal.

Awali akitoa salamu za Chama cha ACT Wazalendo Mshauri wa Chama hicho, Juma Sanani amesema kuwa Wazee ndio kila kitu kwenye uongozi hivyo vijana wanapopewa ushauri wanatakiwa kuuzingatia kwani chama hicho hakina maslahi kwa mtu binafsi bali kwa wanachama wote.

Aidha, amewaomba wasimamizi wa uchaguzi huo kuhakikisha unakua wa huru na haki na kuzingatia ubora na viwango vya kimataifa, huku akiwataka wazee hapo kutumia hekima na busara katika kuhakikisha wanachagua viongozi bora watakaoongoza chama kwa maslahi ya Taifa.

Miongoni mwa wageni waalikwa katika mkutano huo ni pamoja na Sheikh Issa Ponda amesema kuwa wazee wana mambo mengi hivyo vijana wanaposhauriwa ni busara kuwasikiliza kwani hata wakiandika vitabu watu wakavisoma wataweza kujifunza vitu vingi sana.

“Wazee ndio chimbuko la fikra nzuri kwa hiyo wanatakiwa washirikishwe kwenye kila jambo, uchaguzi makini uzingatie uhalisia tunaoufahamu kuweni mfano mzuri wa kuigwa”amesema Sheikh Ponda.

No comments