Ads

KONGAMANO KUBWA LA KIBIASHARA KUFANYIKA KIGALI

Image result for picha za mji wa kigali

Na Jacquiline Mrisho
 mwambawahabariblog

Kongamano kubwa la biashara kati ya Tanzania na Rwanda limepangwa kufanyika Mei 20 mwaka huu katika ukumbi wa Serena Hotel ulioko Jijini Kigali Rwanda.

Kongamano hilo limetangazwa rasmi leo na Makamu Mwenyekiti wa Biashara ,Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA), Dr. Kingu Mtemi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu malengo ya mkutano huo.


“Kongamano hili lina lengo la kukuza biashara, uwekezaji pamoja na kuongeza ushirikiano baina ya wafanyabiashara wa Tanzania na Rwanda, ni fursa kubwa sana itakayosaidia kukuza uchumi wa nchi yetu” alisema Dr. Mtemi.

Dr. Mtemi ameongeza kuwa kongamano hili sio ya kukutana na kujadili changamoto na fursa za kibiashara tu bali itashirikisha wafanyabiashara wanaotaka kuonyesha bidhaa zao katika nchi ya Rwanda.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wamiliki wa Malori na Usafirishaji (TATOA), Bw. Emanuel Kakuyu amesema kuwa hii ni fursa nzuri kwa Tanzania kwa sababu Rwanda inapitisha asilimia 80 ya bidhaa zake kwenye bandari ya Dar es Salaam,Tanzania na asilimia 90 ya bidhaa hizo zinasafirishwa na malori kwenda Rwanda kwa hiyo biashara kati ya Tanzania na Rwanda ikiimarishwa,pato la Taifa litaongezeka.

Aidha, Afisa Miradi wa Biashara, Hurbert Kissasi amewataja waandaji wa Kongamano hilo kuwa ni: Chama cha Wafanyabiashara , Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA), Mamlaka ya Maendeleo na Biashara Tanzania (TANTRADE),Chama cha Wamiliki Malori Tanzania (TATOA), 361 Degrees pamoja na Shirikisho la Sekta Binafsi Rwanda (PSF).

Rai hii ya kushirikiana kibiashara kati ya Tanzania na Rwanda ilitolewa  Machi 6 mwaka huu na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Rais Paul Kagame wa Rwanda walipokuwa wanazindua daraja la Rusumo na kituo cha pamoja cha kibiashara kilichopo mpakani mwa Rwanda na Tanzania.

Kwa kipindi cha miongo kadhaa Rwanda imekuwa mshirika mkubwa wa Tanzania kibiashara katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati. Hivyo Kongamano hili litakuza ushirikiano huu na kuleta tija kwa pande zote mbili ambao ni wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.


No comments