MAPATO TRA YAONGEZEKA ASILIMIA 2.0I, WAKUSANYA TRILIONI 7.99
Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi Bw. Richard Kayombo akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam.
Waandishi wa habari wakiwa katika mkutano wa Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi Bw. Richard Kayombo leo jijini Dar es Salaam.
Na Noel Rukanuga, Dar es Salaam.
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekusanya shilingi trilioni 7.99 katika kipindi cha miezi sita ya mwaka wa fedha 20I8/20I9 kuanzia Julai hadi Desemba mwaka wa jana.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi Bw. Richard Kayombo, amesema kuwa makusanyo hayo ni sawa na ukuaji wa asilimia 2.0I ukitofautisha na ukusanyaji wa kipindi hicho kwa mwaka wa fedha wa 20I7/I8 ambapo walikusanya trilioni 7.83.
Bw. Kayombo amesema kuwa katika makusanyo hayo, mwezi Desemba mwaka wa jana makusanyo yaliongezeka kuzidi makusanyo ya miezi yote iliyopita kwa mwaka huo, kwani walikusanya trilioni I.63, huku mwezi novemba walikusanya trilioni I.2I na mwezi Oktoba ikiwa trilioni I.29.
"TRA inawashukuru walipakodi wote kwa kuendelea kulipa kodi kwa hiari na kwa wakati " amesema Bw. Kayombo.
Katika hatua nyengine Bw. Kayombo ameeleza kuwa katika kutatua kero pamoja na malalamiko ya walipakodi, TRA imeweka utaratibu kwa kila siku ya Alhamisi kuwa ni siku kwa ajili ya mameneja wa mikoa, wilaya kusikiliza na kutatua changamoto za walipakodi.
Amesema kuwa licha ya kutenga siku ya Alhamisi kwa ajili ya kusikiliza kero za walipa kodi, TRA tayari imeanzisha kituo cha ushauri kwa walipakodi kwa Mkoa wa Dar es Salaam kwa lengo la kuongeza ufanisi pamoja na kuwa karibu na walipakodi.
"Tutaendelea kufungua vituo katika mikoa mingine ili kuongeza ufanisi katika utendaji" amesema Bw. Kayombo.
Amefafanua kuwa TRA inaendelea kuongeza wigo kwa walipakodi kwa kuanza kampeni ya usajili wa walipakodi wapya kwa kuwapatia namba ya utambulisho ya mlipakodi (TIN) bure katika maeneo yanayofanyika biashara.
Bw. Kayombo amesema kuwa kwa wafanyabiashara wadogo wadogo wanatakiwa kuchangamkia fursa ya vitambulisho vya wamachinga ambavyo vinapatikana nchi nzima katika Ofisi za wakuu wa mikoa na wilaya kwa shilingi 20,000.
"Vitambulisho vya wamachinga ni maalum kwa wale ambao mauzo yao ghafi hayazidi shilingi 4,000,000 kwa mwaka" amesema Bw. Kayombo.
Hata hivyo Bw. Kayombo amewakumbusha wamiliki wa majengo kulipa kodi ya majengo ambayo viwango vyake ni sh I0,000 kwa nyumba ya kawaida, Sh 50,000 kwa kila sakafu, huku sh 20,000 wakilipa kwa ghorofa za wilayani na jijini.
Mkurugenzi huyo ametoa wito kwa walipakodi na wananchi kuendelea kulipa kodi kwa hiari kwa ajili ya maendelea ya nchi yetu.
Post a Comment