DKT. POSSI AIPONGEZA UNESCO KUPUNGUA KWA UKATILI DHIDI YA ALBINO
Mwambawahabari
Naibu Waziri (Ofisi ya Waziri Mkuu), Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu, Dkt. Abdallah Possi amelipongeza Shirika la Umoja wa Mataifa la Sayansi, Elimu na Utamaduni (UNESCO) kwa kusaidia kutoa elimu kwa wananchi kuhusu watu wenye ualbino pamoja na kufanya tathmini jinsi wananchi walivyo na uelewa kuhusu watu hao.
Dk. Possi ameyasema hayo katika mkutano wa kuelezea tathmini ambayo imefanywa na UNESCO kwa wananchi wa wilaya nne ambazo tathmini ilifanyika na kusema kuwa ni jambo zuri ambalo limesaidia kuonyesha hali jinsi ilivyo na ni njia gani ambayo serikali inaweza kutumia ili kumaliza vitendo vya ukatili kwa watu wenye ualbino.
"Watu wenye ualbino wamekuwa wakiteseka kwa kipindi kirefu, wanakosa nafasi ya kusoma, kufanya biashara na mambo mengi yanawakabili, watu wa mashirika sio suluhisho ni jamii yenyewe, watu wengi bado hawana elimu ya kutosha kuhusu ualbino,
"Inabidi ifike hatua watu wenye ualbino waishi sawa na watu wengine na serikali imekuwa ikifanya jitihada kumaliza vitendo hivyo lakini inabidi jamii itambue hili sio jukumu la serikali peke yake ni muhimu kila mmoja akashiriki kuvitokomeza vitendo vya ukatili, UNESCO imetuonyesha njia ya kuiwezesha serikali kufanikisha nia yake," alisema Dkt. Possi.
Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa UNESCO nchini, Zulmira Rodrigues akizungumza machache kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera,Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira na Walemavu Mhe. Dkt
Abdallah Possi kutoa hotuba kwenye mkutano wa UNESCO unaoangalia tathmini ya watu wenye ulemavu wa ngozi uliofanyika leo katika hoteli ya Protea Courtyard jijini Dar es Salaam. (Habari picha na Zainul Mzige )
Kwa upande wa UNESCO kupitia Mkuu wa Ofisi na Mwakilishi wa UNESCO nchini, Zulmira Rodrigues alisema UNESCO imnatambua kila mwanadamu ana haki ya kuishi kama binadamu wengine na kupitia utafiti wao ambao uliambatana na kutoa elimu wanaamini kuwa ni muda wa jamii kushirikiana ili kutokomeza vitendo vya kikatili kwa maalbino.
"UNESCO imeamua kujihusisha sana na hili jambo na kujitahidi kutoa elimu kwa jamii, tumeanza kulifanyia kazi jambo hili la kikatili kwa maalbino na mashambulizi ambayo wamekuwa wanakutana nayo sababu ya imani za kishirikina ambazo ni kinyume na haki za kibinadamu,
"Utafiti huu utaweza kusidia kumaliza vitendo vya kikatili kwa watu wenye ualbino, kila mtu ana haki za kimsingi na hilo ndilo ambalo UNESCO inalisimamia, na katika kufanikisha hili kila mtu katika jamii kwa nafasi yake ana wajibu wa kushiriki kumaliza vitendo hivi, ni lazima kushirikiana kumaliza jambo hili," alisema Rodrigues.
Tathmini hiyo imefanyika katika wilaya nne ambazo ni Misungwi na Sengerema kwa Mwanza, Msalala iliyopo Shinyanga na Bariadi mkoani Simiyu.
Post a Comment