Ads

KATIBU MKUU WIZARA YA HABARI AFUNGUA MDAHALO WA VIJANA KUJADILI HATMA YA AJIRA KWA VIJANA NCHINI

Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Elisante Ole Gabriel akifungua mdahalo wa hatma ya ajira kwa vijana wa Tanzania ulioandaliwa na Shirika la Kimataifa la Ajira (ILO) na kushirikisha vijana kutoka Tanzania Bara na Visiwani leo jijini Dar es Salaam
Na Anitha Jonas
mwambawahabariblog
Vijana wametakiwa kugeuza changamoto kuwa fursa na kuwa na utamaduni wa kujiajiri na kuchapa kazi kwa bidii badala ya kusubiria kuajiriwa huku wakilaumu mamlaka zinazoshughulika na vijana nchini.
Hayo yamesemwa  na Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Elisante Ole Gabriel alipokuwa akifungua Mdahalo wa siku mbili kujadili  Hatma ya  Ajira kwa Vijana Tanzania uliyoandaliwa na Shirika la Kimataifa la Ajira (ILO) leo jijjni Dar es Salaam.

“Changamoto ya ukosefu wa ajira inaweza kutumika kama fursa kwa kijana anayejitambua kwa kuwa na fikra chanya itakayomuwezesha kutumia elimu aliyoipata kujiajiri bila kuona aibu kufanya baadhi ya kazi mbali ya kuwa amesoma hadi elimu ya juu hivyo kujiongezea kipato,”alisema Prof. Gabriel.
Akizungumza na vijana hao Prof. Gabrieli  amesema kuwa utafiti wa mwaka 2012 kuhusu  idadi ya vijana nchini ulionyesha kuna vijana takribani 16.2 Millioni nchini, na kati ya hao vijana walioajiriwa katika Sekta ya Umma ni Vijana 188,000, Sekta Binafsi Milioni Moja, waliojiajiri wenyewe ni 1.1 millioni  na waliojiajiri  katika sekta ya  Kilimo ni vijana 13.2 milioni.
Aidha Prof. Gabriel amesema kuwa vijana wanatakiwa kujitahidi kukimbizana na teknolojia kwani ukuwaji wa utandawazi katika ulimwengu sasa umekua wa kasi  hivyo kupambana kukabiliana na changamoto hiyo katika soko la ajira.
Kwa upande wa Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Kimataifa la Ajira (ILO) nchi ya Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi na Rwanda Bi. Mary Kawar amesema kuwa shirika hilo liko tayari kuwajengea uwezo vijana katika masuala ya ajira ili kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana.
Naye mshiriki wa mdahalo huo Bw. Masson Kimbo ameiomba serikali kupitia mifumo ya elimu nchini itakayowawezesha vijana kujengewa uwezo wa kujiajiri na kuwa na fikra pana katika masuala ya ujasiriamali.


No comments