Utaratibu wa ajira kwa watanzania wanaofanya kazi za ndani katika nchi za Mashariki ya Kati kuangaliwa upya
Na. Immaculate Makilika
Mwambawahabari
Watanzania 5600 wanakadiriwa kufanya kazi katika kada za madaktari, walimu, wauguzi, wahadhiri, wapishi, wahudumu wa mashambani na bustani na watumishi wa nyumbani, na kati ya hao karibu watanzania 200 ndio wanaofanyakazi za ndani katika nchi za Mashariki ya Kati.
Kada inayofanya kazi za ndani ndio inayopata changamoto nyingi huko ugenini ikiwemo ujira mdogo na vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji. Jambo hili halipaswi kufumbiwa macho. Hata hivyo zipo jitihada za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambazo zimefanyika kupunguza ama kuondoa hali hii.
Kufanya kazi nje ya nchi bila mateso au manyanyaso ni haki ya binadamu kama inavyoainishwa katika mikataba ya kimataifa.
Katika makala hii utaweza kuona baadhi ya vipengele vya mikataba hiyo.
Mkataba wa kimataifa wa haki za kiraia na kisiasa wa mwaka 1966, unataja haki mbalimbali za kiraia zinazolindwa na mkataba huo ikiwa ni pamoja na haki ya kutopewa mateso au kufanyiwa ukatili au vitendo vya kikatili na udhalilishaji ikiwemo hukumu za kikatili katika ibara ya 7. Uhuru wa mtu na usalama wake katika ibara ya 9 na uhuru wa mtu kwenda atakako na kuchagua mahala pa kuishi katika ibara 12.
Katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Ibara ya 17 Kifungu cha (1) kinampa haki raia wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kwenda kokote ndani na nje ya nchi bila kuvunja sheria za nchi.
Kwa misingi hiyo watanzania wanapata fursa za kwenda nje ya nchi, hususani nchi za kiarabu kwa lengo la kufanya kazi za ndani ili kujiongezea kipato na kuweza kuinua uchumi wa familia zao na pamoja na taifa kwa ujumla.
Lakini jambo linalovutia idadi kubwa ya watanzania kwenda kufanya kazi katika nchi za Mashariki ya Kati ambazo ni Omani, Saudi Arabia, Qatar, Bahrain, Kuwait, Lebanon, Syria, Iran, Iraq na Yemen pamoja na nchi zinazounda Falme za kiarabu ambazo ni Abu dhabi, Dubai, Ajman, Al Ain, Fujuirah, Ras al Khaimah na Sharjah ni uhusiano wa karibu sana ambao ni wa kihistoria na kidamu, ambapo nusu ya familia za Oman asili yake ni Tanzania na hivyo kufanya kuwa na mwingiliano wa karibu.
Lakini pia, nchi hizi kwa kiasi kikubwa ni tegemezi ya nguvu kazi kutoka nje ya eneo hilo na hivyo kusababisha soko kubwa la ajira katika maeneo mbalimbali kama vile madaktari, wauguzi, madereva, wapishi, wahudumu wa saluni, watumishi wa shambani na hasa watumishi wa nyumbani(house maids).

Post a Comment