WATAFITI WAIPIGIA CHAPUO SEKTA ISIYO RASMI.
Katika muendelezo uleule Vyuo
vikuu nchini vinafanya tafiti kila iitwapo leo na matokeo ya tafiti hizo
zimelisaidia Taifa katika utatuzi wa changamoto mbalimbali nchini.
Hivi karibuni Chuo Kikuu cha
Mzumbe kwakushirikiana na Chuo Kikuu cha Nairobi na Roskilde cha nchini Denmark
kikiangazia zaidi na kupaza sauti yake juu ya sekta isiyo rasmi na kutoa
mapendekezo kwa serikali na wadau ili kuisaidia sekta hiyo ambayo ni mhimili wa
uchumi nchini.
Vyuo hivyo vitatu vimefanya
utafiti wa aina moja katika mataifa yao na kuziibua changamoto zinazoikumba
sekta binafsi na kutoa mapendekezo ili kuzipatia suluhu changamoto hizo.
Utafiti huo wa miaka minne
uliofanywa na Chuo Kikuu Mzumbe kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Nairobi,
Kenya na Roskilde cha nchini Denmark umependekeza kuwepo kwa sera na taratibu
madhubuti zitakazopelekea sekta isiyo rasmi kupitia vyama vyao kufaidika na
huduma za hifadhi ya jamii.
Malengo makuu ya utafiti huo yalilenga
kufahamu namna wafanyakazi wasio rasmi kwenye sekta za usafiri, ujenzi na
wafanya biashara wadogo Kenya na Tanzania wanavyopata huduma rasmi na zisizo
rasmi za hifadhi ya jamii, bima za afya, pensheni, fursa za mikopo, mafunzo
mbalimbali kama ya afya na usalama na namna vikundi walivyojiundia
vinavyosaidia katika juhudi hizo.
Utafiti huo “Sekta Isiyo Rasmi na
Hifadhi ya Jamii” ulioanza 2017-2020 ulifadhiliwa na shirika la kimataifa la
maendeleo la Denmark (DANIDA) na kufanywa katika miji ya Dar es Salaam, Dodoma,
Nairobi na Kisumu.
Akiongea wakati wa warsha ya
kuwasilisha matokeo ya utafiti huo kwa wadau mbalimbali jijini Dar es Salaam
mwishoni, Mtafiti na Mratibu Mwandamizi katika Utafiti huo kutoka Chuo Kikuu
Mzumbe, Dk Godbertha Kinyondo, anasema upo umuhimu kwa taasisi za serikali na
wadau kujifunza na kushirikiana na vyama vya wafanyakazi wasio rasmi katika
kutunga sera za hifadhi za jamii ili waweze kufaidika na huduma muhimu za
kijamii.
Dk Godbetha anasema ni muhimu
sasa kwa serikali kupitia taasisi zake mbalimbali kujenga uwezo na kushirikisha
vyama vya wadau hao katika kutunga sera zinazogusa maisha yao na kupitia upya
programu za hifadhi za jamii ili zikidhi mahitaji mapana ya wafanyakazi hao
katika sekta isiyo rasmi, hususani ya usafirishaji inayokua kwa kasi Tanzania
na Afrika ya Mashariki kwa ujumla.
“Serikali ipange kuwa na huduma
stahiki za hifadhi ya jamii na rahisi inayoendana na hali halisi kwa
wafanyakazi wa kada hii katika sekta ya usafirishaji,” alisema Dkt. Kinyondo.
Mtafiti mwingine wa Chuo Kikuu
Mzumbe, Aloyce Gervas anasema sekta ya ujenzi ambayo ni miongoni mwa sekta
muhimu katika kuchangia pato la taifa kwa asilimia 13 bado ina watu wasio na
ujuzi rasmi. Sekta hiyo pia ndio
inayoongoza katika kusababisha ajali za kazini kwa asilimia 23.7 kulinganisha
na sekta nyingine.
Hivyo basi Dk Godbetha anaona
kabisa kuwa upo umuhimu wa kupitia upya sera ya taifa ya sekta ya ujenzi ili
kuwatambua vyema mafundi ujenzi wasio na taaluma rasmi na mifuko ya hifadhi ya
jamii kama NSSF kutoa elimu ya kutosha kwa mafundi nchini juu ya faida za
mifuko hiyo.
“Sera ya Afya na Usalama mahali
pa kazi irejewe ili kutambua watu wasio rasmi wanaofanya kazi katika maeneo
rasmi kama wajenzi,” alisema.
Mtafiti Mwandamizi toka Chuo
Kikuu cha Nairobi, Prof. Winnie Mitullah alisema juhudi za kuboresha sekta
isiyo rasmi zinahitaji ushiriki wa wadau mbalimbali na ushirikiano kati ya nchi
na nchi ili kufanikiwa.
“Ni muhimu watafiti, maofisa wa
serikali, wadau wa maendeleo, wafanyakazi sekta isiyo rasmi kukaa na kuja na
suluhisho litakalokuwa endelevu kwa faida ya nchi zetu,” anasema
Mtafiti, Anne Kamau wa Chuo Kikuu
Nairobi anasema suala la hifadhi ya jamii kwa sekta isiyo rasmi bado ni
changamoto kubwa nchini Kenya.
“Eneo hili linahitaji mjadala
mpana utakaohusisha wadau wengi zaidi ili kuhakikisha sekta isiyo rasmi
inafaidika na huduma za hifadhi ya jamii kwa kiasi kikubwa,” anasema Anne.
Akichangia, wakati wa mrejesho wa
utafiti huo Rehema Hassan Chuma, Meneja, Kitengo kinachoshughulikia sekta isiyo
rasmi, Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) anawapongeza watafiti kwa juhudi
zao zakufanya utafiti huo na kusema tayari shirika hilo linafanya kazi ya
kuongeza wigo wa wanachama kupitia sekta isiyo rasmi tangu mwaka 2018.
“Tutaisaidia serikali kuhakikisha
kuwa sera ya hifadhi ya jamii kwa sekta isiyo rasmi inakamilika,” anasema. Hata
hivyo anashauri kuwa umefika wakati sasa kwa makundi kama madereva bodaboda,
daladala na wajenzi kujirasimisha katika vyama vitakavyotambulika na kufaidika
na huduma kama hifadhi za jamii, na mikopo.
Kwa upande wake Gaston Kikuwi,
Mwenyekiti wa chama mwamvuli wa vyama vya sekta isiyo rasmi Tanzania (VIBINDO)
chenye vyama 741 na wanachama zaidi ya 68,000 nchini anasema mjadala wa huduma
za hifadhi ya jamii kwa wafanyakazi sekta isiyo rasmi ni muhimu sana kwa
maendeleo ya nchi.
“Panatakiwa dhamira ya kweli
katika kutekeleza mapendekezo ya utafiti huu kwa faida ya nchi yetu,” anasema Kikuwi.
Awali, akifungua warsha hiyo kwa
niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe, Prof. Lughano Kusiluka; Dkt. Mary
Rutenge anasema utafiti huo unaolenga kuboresha maisha ya wananchi katika nchi
hizo mbili ni muhimu na kushauri mamlaka husika kufanyia kazi mapendekezo yake.
Kati ya matokeo mengine muhimu ya
utafiti huo ni kuchapishwa kwa kitabu kuhusu hifadhi ya jamii na sekta isiyo
rasmi Kusini mwa Jangwa la Sahara kikiangazia mifano halisi katika nchi za
Tanzania na Kenya. Uzinduzi wa kitabu
hicho ulifanyika katika warsha hiyo.
Pia, utafiti huo umepelekea kupatikana kwa wanazuoni wawili ngazi ya
uzamivu Tanzania na Kenya.
Kwa upande wake mwendesha
pikipiki mkazi wa Yombo Vituko kwa Ali Mboa anasema wao wapo tayari kujiunga na
kila mfumo wowote na hata kuchangia fedha kwa ajili ya akiba yao ya kesho
lakini anasema shida inakuja unapohitaji huduma kwa wakati muafaka.
‘’Sisi kujiunga na kitu chochote
chenye manufaa hapa kijiweni kwetu si tatizo ni kijiwe cha waendesha pikipiki
tunaojielewa na kujitambua na tunalisha familia zetu na kujikimu kupitia kazi
hii shida inayokuja wakati tunapohitaji huduma kuipata kwa wakati nikupe mfano
kwenye bima tumekata hizo bima sijui NHIF iliyoboreshwa lakini kupata dawa sasa
katika hospitali teule ni mtihani kikubwa watoa huduma wawe makini katika utoaji huduma na wajali wateja
wao sisi ndiyo tunao waweka’’anasema
Kwa upande wake Stephen Chadinga
anayejishughulisha na masuala ya Ujenzi katika daraja la Tanzanite Dar es
Salaam anasema upo umuhimu wakujiunga na mfumo rasmi kwani hawajui kesho yao.
‘’Kwa sasa huwezi ona umuhimu wa
hili lakini shida inapokukuta sasa ndiyo utajua umuhimu wakae lakini pia mfano
mfuko wa fidia kwa wafanyakazi ukoleze makali katika kukusanya michango yote
kwa waajiri mana michango haipelekwi kwa wakati na hata wakati mwingine
unapopata ajali kazini gharama za matibabu ni mtihani,, anasema
Jumla ya madereva daladala 250 na
waendesha bodaboda 158 walihusishwa katika utafiti huo Tanzania, wakati wajenzo
212 walihusishwa. Kwa upande wa Kenya,
wafanyakazi 200 katika sekta ya usafirishaji walihusishwa katika utafiti huo.
Post a Comment