Ads

Wawekezaji wa Uturuki Wawasili nchini Kuangalia Fursa za Uwekezaji

Balozi wa Uturuki nchini Tanzania Mh.Ali Davutoglu akifuatilia mkutano .

Na.Grace Semfuko-MAELEZO

Balozi wa Tanzania Nchini Uturuki Profesa Elizabeth Kiondo na Balozi wa Uturuki Nchini Tanzania Ali Davuto Glu wameongoza ujio na mapokezi ya Wawekezaji wa makampuni saba makubwa ya Nchini Uturuki ambao wamewasili nchini kwa ajili ya kuangalia maeneo ya uwekezaji wa Viwanda ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya tano inayohimiza Sera ya Viwanda kuelekea uchumi wa kati.

Wawekezaji hao wameonesha nia ya kuwekeza kwenye maeneo mbalimbali ikiwepo viwanda, Kilimo na Sekta ya umeme, ambapo mikoa ya Dodoma na Simiyu imepewa kipaumbele na wawekezaji hao ambao wataanza zoezi hilo la ujenzi wa viwanda ifikapo mwezi Juni mwaka 2019.

Akizungumza katika kikao cha pamoja cha wawekezaji hao na Kituo cha uwekezaji Tanzania TIC Balozi wa Tanzania Nchini Uturuki Profesa Elizabeth Kiondo alisema hatua ya wawekezaji hao kuonesha nia ya kuwekeza nchini inatokana na mazingira mazuri ya uwekezaji yaliyopo nchini pamoja na juhudi za kuwahamasisha.

“Ndugu zangu Wawekezaji hawa wamekuja wakati muafaka kabisa wakati ambao Serikali yetu inahimiza uchumi wa viwanda,pia ni kwa sababu Serikali yetu imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji,lakini pia tumekuwa tukiwahamasiaha waje kuwekeza hapa kwetu Tanzania” Alisema Balozi wa Tanzania Nchini Uturuki Profesa Elizabeth Kiondo.

Alisema bado wana kazi kubwa ya kuhamasisha wawekezaji wa kutoka Uturuki kuja Tanzania kuwekeza kwenye sekta mbalimbali na hivyo ujio wao ni mwanzo tu wa wawekezaji wengine kuja kuangalia fursa na mazingira yaliyopo.

Nae Balozi wa Uturuki Nchini Tanzania Ali Davuto Glu alisema Tanzania inaelekea kufikia malengo makubwa ya kiuchumi hali inayoungwa mkono na Serikali ya Uturuki na kuamua kuwahamasisha wawekezaji wa nchini humo kuja kuwekeza Tanzania.

“Tanzania inafikia malengo ya kiuchumi  iliyokusudiwa, Sisi Uturuki tunaunga mkono mambo yote ya kukuza uchumi yanayofanywa na Serikali ya Tanzania, katika kuhakikisha inapiga hatua za kiuchumi tumeamua kuwahamasisha  wawekezaji hawa waje wawekeze” alisema Balozi Davuto Glu.


Kwa upende wake Mkurugenzi wa uhamasishaji na Uwekezaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania TIC John Mnali alizitaka taasisi zinazohusina na maeneo ya uwekezaji kutoa ushirikiano kwa wawekezaji hao ili kurahisisha kazi hiyo kufanywa kwa wakati.

No comments