Ads

MGOMBEA WA CCM APEWA FOMU

Mgombea wa Ubunge kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Timotheo Mnzava juzi alichukua fomu huku akisema kuteuliwa kwake na CCM kupeperusha bendera ya chama hicho katika jimbo la Korogwe Vijijini ni neema na mapenzi ya Mungu.
Akizungumza baada ya kukabidhiwa fomu yake na ofisa msaidizi wa uchaguzi wa jimbo hilo, Samina Gullam, mgombea huyo alisema kupitishwa kwake katika kundi la wagombea 44 licha ya kushika nafasi ya tatu, uteuzi wake ulikuwa na baraka za Mungu.
"Nikiwa Arusha nikasikia Kamati Kuu imeniteua kuwa mgombea wake, baada ya hapo nilipiga magoti chini kumshukuru Mungu kuonyesha ishara ya kutambua mapenzi yake kwangu," amesema Mnzava.
Aliwataka wagombea wote wawe na fikra na msimamo wa chama hicho wamuunge mkono ikiwemo wanachama waliokuwa wakiwaunga mkono ili kulinda maslahi ya chama hicho katika uchaguzi huo utakaoanza kampeni Agosti 21 mwaka huu.
Mmoja wa wagombea katika kinyang'anyiro hicho, Shebila Idd alisema kuwa ni wakati wa kuvunja makundi na wamsaidie mgombea huyo ili kuiwezesha CCM kushinda tena kwenye jimbo hilo.
"Maneno ya ukabila au dini hayana nafasi tuhakikishe tunamnadi mgombea wetu na kushinda jimbo la Korogwe Vijijini, tusiyumbe tuunge mkono maamuzi ya chama chetu," alisema Shebila ambaye ni Diwani Kata ya Kerenge.
Awali akimkabidhi fomu hiyo Gullan alisema licha ya mgombea huyo wa CCM kuchukua fomu, wagombea wengine waliochukua ni pamoja na Abdul Aziz wa Chama cha AAFP na Josephine George wa chama cha DP.
Uchaguzi huo utafanyika Septemba 16 mwaka huu kutokana na kifo cha Stephen Ngonyani aliyefariki dunia Julai 2 na kuzikwa tarehe 4 kijijini kwake Kwamndolwa wilayani hapa.

No comments