VIGOGO NEMC KUPANDISHWA KIZIMBANI
Na mwandishi wetu
Maofisa Mazingira wawili wa Baraza la Taifa la Mazingira (NEMC), wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wanakabiliwa na mashitaka matatu likiwemo la kughushi.
Washitakiwa hao ambapo walifikishwa mahakamani hapo leo ni Andrew Kalua na Arnold Kisiraga.
Mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi, Wakili wa Serikali, Narindwa Sekimanga, aliwasomea washitakiwa mashitaka ya kula njama ya kutenda kosa, kughushi na kuwasilisha nyaraka ya kughushi.
Washitakiwa hao wanadaiwa tarehe tofauti kati ya Machi Mosi na Julai 31, mwaka huu maeneo ya Mikocheni, wilayani Kinondoni, Dar es Salaam, walikula njama pamoja na mtu mwingine ili kufanya kosa la kughushi.
Shitaka la pili, washitakiwa hao wanadaiwa kati ya Machi Mosi na Julai 7, mwaka huu, Mikocheni, Dar es Salaam, kwa nia ya kudanganya walighushi nyaraka.
Inadiwa walighushi nyaraka hiyo ambayo ni mukhtasari kwa kamati ya ushauri ya sekta mbalimbali iliyopitia kikao cha kampuni ya East Coast Liquid storage Limited iliyoko kwenye kiwanja namba 231, maeneo ya Kurasini, Temeke , Dar es Salaam ya Juni 16, mwaka huu kuonesha kamati ya ushauri wa kitaalamu iliyokaa Aprili 11, mwaka huu katika ukumbi wa NEMC na kuazimia wazungumzia upungufu ulioonekana, hukumu wakijua sio kweli.
Mshitakiwa Kalua anadaiwa Juni 16, mwaka huu, aliwasilisha nyaraka hiyo ya kughushi kwa Cecilia Toto Douglas.
Washitakiwa hao walikana mashitaka hayo ambapo upande wa jamhuri ulidai upelelezi haujakamilika.
Hakimu Shaidi alitoa masharti ya dhamana ambapo kila mshitakiwa alitakiwa kuwa na wadhimini wawili wenye barua ambapo kila mmoja atatia saini dhamana ya sh. milioni tano.
Washitakiwa walitimiza masharti ya dhamana na kuachiwa huru hadi Januari 11, mwakani itakapopelekwa kwa kutajwa.

Post a Comment